KATUMENI YALIA UKOSEFU WA ELIMU YA MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA.




Ukosefu wa elimu ya matumizi ya nishati safi  ya kupikia bado ni changamoto inayopelekea baadhi ya wakaazi wa Katumeni Shehiya ya Makombeni, kuendelea kutumia kuni kama ni nyenzo kuu ya kukidhi mahitaji.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi mwanajamii Mtumwa Abdallah Mohammed na Mohammed Faki Ali, wamesema hawajawahi kufikiwa kupewa elimu hiyo hali inayowapa ugumu kutumia nishati safi ya kupikia katika kuandaa chakula cha siku.

Matumizi ya nishati safi ya kupikia hasa vijijini inahitaji elimu ya kutosha kwani hatuna uzoefu na utumiaji wake,kufanya hivyo kutatupa urahisi wa kutumia sambamba na kujikinga na madhara yatokanayo na matumizi ya nishati isiyo salama” walisema wanajamii.

Mwashumu Makame Haji,Sheha wa Makombeni amekiri kuwepo kwa changamoto hiyo Shehiyani hapo, amechukua nafasi kuielimisha jamii kwa kusema

“Gesi haina madhara kama jamii inavyoeleza, hivyo ni vyema kwa  taasisi husika kupunguza gharama ili wanajamii wa vijijini waweze kutumia”. Alisema sheha wa Makombeni.

Moh’d Faki Saleh ,daktari kutoka Hospiali ya Abdallah Mzee Mkoani, amekiri kuwepo athari lukuki zinazosababishwa na utumiaji wa kuni na kuongeza….

“Ni vyema kila mmoja kusimama kwa nafasi yake kuhakikisha wanawake wananusurika kiafya kutokana na matumizi ya kuni”.aliongeza dkt Mohammed.

Aisha Abdalla Rashid afisa bayoanway idara ya mazingira pemba amekiri uwepo wa wananchi wengi kutokua na elimu hiyo na kuamini kua nishati safi ya kupikia ni gesi tu.

“Mbali ya nishati ya gesi umeme , Bayo gas na makaa ya takataka nazo ni salama kwa kupikia , hivyo ndani ya miezi sita ijayo wananchi wote wa Mkoani wataweza kufikiwa ili kupatiwa elimu hiyo”.Alisema  

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan akizindua Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia mwaka huu, Amesema nguvu kubwa ya taifa inaathirika  kiafya kwa matumizi ya kuni na Makaa.

Kwani, watanzania zaidi ya 33,000 hupoteza maisha kila mwaka kwa tatizo la mfumo wa kupumua ambao huchangiwa na matumizi ya kuni za kupikia wanawake wakiongoza kwenye idadi hiyo.

Shehiya ya Makombeni,ina zaidi ya wakaazi 2100 ambapo takriban asilimia 90 wanatumia kuni kwa kupikia.

                   

Picha kwa msaada wa mtandao. 

Comments